Askari ajikung’uta risasi ya koromeo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, George KyandoASKARI wa Gereza la Kitete lililopo katika wilaya ya Nkasi katika mkoa wa Rukwa, Sajini Faustine Mwakyonike (39), amejiua kwa kufyatua risasi kwenye koromeo lake na risasi kutokea utosini akiwa lindoni usiku wa kuamkia juzi Jumamosi.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, George Kyando amethibitisha mkasa huo na kwamba uchunguzi unafanywa ili kubaini chanzo cha askari huyo kujiua.

“Tukio hilo ni la kweli askari huyo wa Magereza kweli amejiua ila kwa sasa sina taarifa zaidi za kina kwa kuwa niko safarini …ila uchunguzi wa kubaini chanzo cha askari huyo kujiua unaendelea na taarifa itatolewa,” alieleza Kamanda Kyando.

Akisimulia tukio hilo, Mkuu wa Gereza la Kitete, Job Lwesya alisema Sajini Mwakyonike aliingia zamu Ijumaa saa nne usiku, na alikuwa lindoni katika gereza hilo akiwa na bunduki.

“Muda mfupi baada ya saa sita usiku askari huyo alijiua kwa kujipiga risasi na kufa papo hapo …alitumia bunduki aliyonayo kujiua alielekeza mtutu wa bunduki kwenye koromeo kisha akaifyatua na risasi ilitokea utosini mwake,” alieleza Lwesya.

chanzo;habarileo.

Comments