MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema mtu yeyote
atakayebainika kuiba au kuharibu vyuma vilivyowekwa katika bustani za
pembezoni mwa barabara za mkoa huo atalazimika kununua vyuma 10 kama
fidia.
Makonda alitahadharisha hivyo jijini humo wakati alipofanya ziara
wilayani Kinondoni kujionea hali ilivyo katika bustani mbalimbali
zilizowekewa uzio wa vyuma. Ukaguzi wa bustani hizo ni maandalizi
kuelekea kwenye uzinduzi wa Kampeni ya Mti Wangu itakayofanyika Oktoba
mosi.
Alisema lengo la Serikali ni kuona jiji hilo linakuwa na muonekano wa
kuvutia na kwamba hatamvumilia yeyote atakayeiba vyuma hivyo na
atakayeharibu mazingira.
“Kuna watu hawajazoea kuona mambo mazuri, tunatengeneza ili
kupendezesha jiji halafu wao wanawaza kuiba vyuma vya bustani na
kuharibu mazingira. Atakayekamatwa atalipa vyuma 10 kwa kila chuma
alichokiiba au kuharibu,”Makonda alisema.
Aidha, alisema baada ya kukamilisha kutengeneza bustani hiyo,
watalazimika kuweka taa pamoja na nyaya za shoti ili kuzuia wananchi
watakaotaka kufanya uharibifu.
Pia, alisema bustani hizo zitakuwa na maji safi kutoka Mamlaka ya
Majisafi na Majitaka (Dawasco) ambayo yatatumika kumwagilia kuliko
kusubiri kipindi cha mvua pekee au kupeleka maji kwa kutumia magari.
Makonda pia aliwataka wakazi wa jiji hilo wenye kampuni pembezoni mwa
barabara kuchukua jukumu la kuzitunza bustani hizo na watapewa mita za
maji kila mmoja, ikiwa ni pamoja na jukumu la kuzisimamia ili
kuhakikisha zinabaki katika muonekano mzuri.
“Lengo ni moja na ushiriki wa kampuni ni muhimu, kampuni zote
zitapewa utaratibu ikiwemo kupewa mita za maji na kuhakikisha bustani
iliyo mbele ya ofisi ya kila kampuni inakuwa na muonekano mzuri,”
aliongeza.
Katika hatua nyingine, Makonda alimtaka Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni,
Ally Hapi kuwatafutia eneo wafanyabiashara wanaouza bidhaa pembezoni mwa
barabara katika eneo la Moroco kwa kuwa eneo wanalolitumia kwa sasa si
halali kwa biashara.
Kwa upande wake, Hapi alisema wilaya hiyo itapanda miti zaidi ya 5000
na kwamba kwa sasa wanaendelea kufunga miundombinu ya maji na kuchimba
mashimo kwa ajili ya kupanda miti hiyo.
chanzo;habarileo.
Comments