UN: Tanzania ni ya mfano elimu kwa wote.

KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon amesema utashi wa kisiasa, matumizi ya Pato la Taifa na matumizi ya fursa mbalimbali unaifanya Tanzania kuwa moja ya nchi ya mfano katika uboreshaji na upatikanaji wa elimu kwa wote.

Ban Ki-moon aliyasema hayo juzi wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ripoti ya Kamisheni ya Kimataifa kuhusu, “Kizazi kinachojifunza: Uwekezaji katika elimu kwa dunia inayobadilika” iliyofanyika katika Makao Makuu ya UN na kuhudhuriwa karibu na makamishna wote wanaounda tume hiyo akiwamo Rais mstaafu, Jakaya Kikwete.

Tume hiyo ambayo ipo chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu mstaafu wa Uingereza ambaye pia ni Mjumbe Maalumu wa Katika Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Elimu, David Cameroon inawahusisha pia baadhi ya marais waliopo madakarani, mawaziri wakuu waliopo madarakani na waliostaafu.

Wengine ni Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Dunia, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), wawekezaji wakubwa akiwamo tajiri namba moja Afrika, Aliko Dangote, taasisi za utafiti, wataalamu wa masuala ya fedha, asasi za kijamii na makundi ya vijana wakiwamo wanafunzi.

“Uzoefu wa nchi kama Tanzania, Vietnam na nchi yangu mwenyewe Korea, unaonesha kwamba pale ambapo pana utashi wa kisiasa, ukijumuishwa na uwepo wa fursa na raslimali fedha kuna kitu kinachoweza kufanyika katika elimu,” alisema Ki-moon.

Na kutokana na uzoefu wa nchi kama Tanzania na nyinginezo, mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa alisema Jumuiya ya Kimataifa ni lazima iwe tayari kuzisaidia kwa mitaji nchi ambazo zimeamua na kujituma katika kuifanyia mageuzi mifumo yake ya elimu na kujipati matokeo yanayoridhisha.

Akichangia majadiliano ya uzinduzi wa ripoti hiyo, Rais mstaafu Kikwete kama mmoja wa makamishna na ambaye pia aliongoza majadiliano kuhusu kipengele cha tatu cha mapendekezo ya ripoti hiyo kuhusu ujumuishi katika elimu, alisema, “Mafanikio ya elimu lazima yamfikie kila mmoja wakiwamo wale wanaoishi katika mazingira magugumu na wanaobaguliwa wakiwamo wasichana.”

Aliongeza kuwa bahati mbaya leo hii Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, msichana mmoja kati ya 20 wanaoishi katika maeneo ya umaskini ndiyo walio katika hatua za kumaliza elimu ya msingi, na kwamba takribani watoto milioni 75 ambao wamo katika umri wa kwenda shule wanakabiliwa kila siku na hatari moja ama nyingine.

chanzo;mpekuziblog.

Comments