RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, amesema serikali itafanya
kila linalowezekana kuhakikisha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya
wafanyakazi wa vyombo vya habari vya serikali yanaimarishwa ili
kurejesha hadhi ya taasisi hizo.
Dk Shein ambaye alitembelea redio na gazeti la Zanzibar Leo na
kufanya mahojiano maalumu na Shirika la Habari na Utangazaji Zanzibar
(ZBC), alisema ameridhishwa na utendaji wa kazi wa viongozi na
wafanyakazi wa vyombo, ambao wamekuwa wakijitahidi kufanya kazi vizuri,
licha ya changamoto wanazokabiliana nazo.
Alisema serikali imedhamiria kufanyia marekebisho makubwa ZBC na
vyombo vyote vya habari vya serikali sio tu kwa kuinua viwango vya
mishahara ya wafanyakazi, lakini pia kutoa tuzo maalumu kila
inapohitajika kwa wafanyakazi watakaofanya kazi vizuri ili kuinua ari na
motisha ya kazi.
Katika hatua za awali za kuziimarisha taasisi za vyombo vya habari
vya serikali, alisema serikali imeshatoa agizo kuitaka Wizara ya Habari,
Utamaduni, Utalii na Michezo, kuandaa posho maalumu kwa wafanyakazi
wanafanya kazi katika mazingira magumu.
Akizungumzia baadhi ya wafanyakazi ambao wameondoka kwenye vyombo vya
habari vya serikali kutokana na maslahi duni na mazingira
yasiyoridhisha, alisema ana matumaini makubwa kwamba wengi wao watarejea
siku zijazo kama ambavyo wamekuwa wakifanya kwenye taasisi mbalimbali.
Rais wa Zanzibar kuhusu Zanzibar Leo alisema, serikali imeshanunua
mitambo mipya ya kisasa ya uchapishaji ambayo itatumika pia kuchapishia
gazeti hilo badala ya kuchapishwa nje ya Zanzibar, jambo linalosababisha
mlundikano mkubwa wa deni la gharama za uchapishaji.
Jumamosi iliyopita, Rais wa Zanzibar alikutana na uongozi wa Wizara
ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Uongozi wa Shirika la Habari na
Utangazaji Zanzibar (ZBC) na wa Zanzibar Leo, kuzungumzia mkakati wa
kusaidia kuimarisha matangazo ya redio na Tv katika Shirika la Habari na
Utangazaji Zanzibar (ZBC).
chanzo;habarileo.
Comments