Nyumba 14,525 hazifai Kagera.

MKUU wa Mkoa wa Kagera, Salum Kijuu amesema tathimini inayoendelea kuhusu athari za tetemeko la ardhi lililotokea mkoani humo Septemba 10, mwaka huu, imebaini kuwa nyumba 2,072 zimeanguka kabisa, nyumba 14,525 zina nyufa kubwa na hazipaswi kuishi watu na nyumba zaidi ya 9,000 zinahitaji kufanyiwa marekebisho.

Aidha, imefahamika kuwa Sh bilioni tisa zinahitajika ili kujenga na kurekebisha makazi ya wananchi wa Kagera yaliyoathiriwa na tetemeko la ardhi kubwa.

Kijuu, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa ya Mkoa alisema hayo wakati akitoa taarifa kwa Kamati ya Maafa Kitaifa katika Ofisi ya Waziri Mkuu ikiongozwa na Waziri wa Nchi, Sera, Bunge, Ajira na wenye Ulemavu, Jenista Mhagama ili kujua maendeleo ya tathimini inayoendelea.

“Mpaka sasa tathimini imebainika nyumba hizi, ambapo tukiamua kutoa mgawo tuliopanga tangu mwanzo wa kila kaya moja kupewa mifuko mitano ya saruji na mabati 20 tukitaka kufanikisha hili ili waathirika waweze kufikiwa wote tunahitaji shilingi bilioni tisa za haraka,” alieleza Kijuu.

Alisema takwimu hizo ni za makazi ya wananchi tu ambao majengo ya taasisi kama vile shule, makanisa, misikiti, vituo vya polisi, zahanati na magereza havijaunganishwa humo, akibainisha kuwa wataalamu wamesema shule moja kama ile ya Ihungo kuirudisha katika hali yake ya kawaida zinahitajika Sh bilioni 4.5.

Alisema mpaka sasa misaada inaendelea kupokewa, na hadi kufikia Septemba 18, vifaa mbalimbali vimepokewa na Kamati ya Maafa ya Mkoa vyenye thamani ya Sh bilioni tano huku zaidi ya Sh milioni 663 zimeishaingizwa katika akauti ya maafa.

Aidha, alisema pia harambee iliyofanyika wiki iliyopita kwa kuongozwa na mkuu wa mkoa fedha taslimu Sh milioni saba zilipatikana na ahadi ikiwa Sh milioni 700.

Katika hatua nyingine, Balozi wa Kenya nchini, Chirau Ali Mwakwere amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali ikwemo mabati 4,000, magodoro100 na mablanketi 400 kwa niaba ya Rais Uhuru Kenyatta, na kueleza kuwa wananchi wao na serikali yao wameguswa sana na tukio hilo ndiyo maana wakajitoa kwa hicho kidogo ili wasaidie.

“Tunakumbuka kauli ya Mwalimu Julius Nyerere aliyotoa kuwa binadamu wote ni ndugu na Afrika ni moja, kwa hiyo sisi ni ndugu inabidi tusaidiane kwa shida na raha,” alisema Balozi Mwakwere na kuipongeza Serikali ya Tanzania kuboresha miundombinu ya barabara kwani wamesafiri kwa njia ya barabara kutoka mwanzo wa safari yao mpaka Bukoba bila usumbufu na kuifananisha barabara hizo na za Afrika usoni.

Wakati huo huo, maofisa elimu wa shule za sekondari na msingi zilizopo mkoani Kagera wamepewa siku tatu kukamilisha taarifa sahihi za majengo yaliyobomoka na idadi ya wanafunzi walioathiriwa na tetemeko huku wakitakiwa kuwa makini katika utoaji wa taarifa za tukio hilo.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako alisema hayo wakati akitembelea shule zilizoathiriwa na tetemkeko na kusababisha majengo kuanguka na nyufa kubwa kutokea katika Wilaya ya Missenyi na Manispaa ya Bukoba.

Shule hizo ni sekondari ya Nkenge, shule ya bweni Bwabuki Nyanshenye, shule za msingi zilizopo wilayani Missenyi pamoja na shule za sekondari za wavulana Ihungo na Nyakato na Shule ya Msingi Mugeza Mseto ambayo ni shule ya wanafunzi maalumu wenye ulemavu mbalimbali zilizopo Manispaa ya Bukoba.

Profesa Ndalichako alisema ikiwa ni siku nane tangu kutokea kwa ajali hiyo, maofisa elimu wangekuwa na taarifa sahihi za majengo yaliyoharibika zaidi na yale yaliyo na nyufa.

“Taarifa hizi zinakuwa kama za kubahatisha, umakini unatakiwa kwa hili, ndani ya siku tatu lazima kupata taarifa ambazo zimechambuliwa vizuri na zenye kuonesha wapi kuna tatizo,” alieleza na kuongeza kuwa katika shule hizo zilizoharibika wanafunzi watatafutiwa sehemu nyingine ya kuendelea na masomo yao wakati shule walizokuwa wakisomea zikijengwa na shule nyingine kufanyiwa ukarabati kwa ubora zaidi.

chanzo;habarileo.

Comments