Mkurugenzi Malinyi ashawishi wasomi kulima mpunga.

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Malinyi, Marcelin Ndimbwa ametekeleza ahadi yake na kuunga mkono maagizo ya serikali ya kuondoa umaskini kwa vijana kwa kushawishi wahitimu 35 wa vyuo vikuu kujiunga na mradi wa kilimo cha mpunga wilayani humo.

Kupitia mpango wake huo, mkurugenzi huyo amewawezesha wasomi hao kuungana na kupewa ekari 45 za kulima zao hilo, lakini akisema watawezeshwa zaidi kwa kupewa mbegu za kisasa bure ambazo zitawawezesha kupata mavuno baada ya siku 85.

Mkurugenzi huyo kwa ushirikiano mkubwa na Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Matiku Majura wamekuwa wakibuni mikakati ya kuwakomboa Watanzania kutokana na agizo la Rais John Magufuli la kuwataka viongozi kusimamia maendeleo ya wananchi katika maeneo yao.

Kwa mujibu wa Msimamizi wa Mradi wa Kilimo cha Umwagiliaji katika Halmashauri ya Wilaya ya Malinyi, ambaye ni Ofisa Kilimo, Mhandisi Maimuna Makutika, wasomi hao watanufaika na kilimo hicho kwa kuzalisha magunia kati ya 40 hadi 50.

Akizungumzia gharama za kilimo hicho, Mhandisi Makutika alisema kilimo hicho ni nafuu kutokana na mkulima kutumia pungufu ya Sh 600,000 hadi mavuno kwa ekari moja na baadaye kupata faida kwa kuuza gunia moja kati ya Sh 80,000 na Sh 120,000.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Ndimbwa alisema kupitia uwekezaji huo, vijana hao watakuwa wamepata ajira ya kudumu lakini pia watakuwa wamejikwamua kiuchumi kama watafanya bidii na kuyatunza mashamba hayo inavyostahili.

Alisema tayari vikundi vya vijana wilayani hapo vimehamasika baada ya kuona mwitikio wa wasomi kuwekeza kwenye kilimo na kwamba mpaka sasa vijana wenyeji walioitikia ni zaidi ya 150, vikundi 30 na ekari zaidi ya 200 zimeshalimwa.

chanzo;habarileo

Comments