MKUU wa Wilaya ya Malinyi mkoani Morogoro, Majura Kasika, ameliagiza
Jeshi la Polisi kusaka na kumchukulia hatua za kisheria diwani wa zamani
wa Kata ya Ngoherenga, Pius Mwalase na Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho,
Novatus Mvogo kwa tuhuma za kutoweka na trekta la kijiji pamoja na
maelfu ya michango ya fedha.
Agizo hilo la kusakwa na kukamatwa kwa watu hao ni baada ya Mkuu wa
Wilaya hiyo kupokea malalamiko ya wananchi wa kata hiyo kuwa tangu
trekta hilo linunuliwe kwa mkopo wa Sh mil 50 kutoka Shirika la
Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA –JKT) mwaka 2012/2013
halipo kijijini hapo.
Wananchi hao walidai kuwa waliokuwa viongozi wa Kata ya Ngoherenga
kwa kushirikiana na kijiji hicho hawakuwahi kusoma mapato na matumizi ya
mradi wa trekta hadi sasa na kwamba trekta hilo halijilikani lilipo.
Walidai kwa nyakati tofauti kuwa viongozi hao wa zamani akiwemo
aliyekuwa diwani wa kata pamoja na mtendaji wa kijiji walitoroka na mali
mbalimbali za kijiji ikiwemo fedha za michango Sh mil 1.1.
Fedha hizo na matumizi yake katika mabano ni Sh 442,000 (mchango wa
umeme ), Sh 110,000 (michango ya matofali) na nyingine zikiwa ni fedha
za kijiji Sh 585,000 pamoja na trekta lililonunuliwa kwa njia ya mkopo
kutoka SUMA-JKT.
Kutokana na malalamiko hayo, Mkuu wa wilaya hiyo alitoa maagizo ya
serikali ya wilaya kwa kuagiza vyombo vya dola kuwatafuta mara moja ili
hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.
Katika hatua nyingine, aliwahakikishia wananchi wa Malinyi kuwa hatua
mbalimbali zimechukuliwa kwa kuanzisha doria katika barabara ya
Lupiro-Malinyi ili kukabiliana na majambazi wanaofanya vitendo vya
utekaji wa magari ya abiria na mizigo.
chanzo;habarileo.
Comments