Nishati wajipanga umeme usikatike Dodoma.


 

WIZARA ya Nishati imesema imejipanga kuhakikisha Dodoma inakuwa na umeme wa uhakika wakati nchi itakapohamia rasmi ili kukidhi mahitaji kutokana na ongezeko la watu litakalotokea mkoani humo.
“Sasa tunajipanga kuhakikisha kunakuwa na umeme wa kutosha kuondokana na habari za kukatika katika kwa umeme kwani uwepo wa makao makuu utaongeza matumizi ya umeme kutokana na idadi ya watu kuongezeka na hata ujenzi utaongezeka.”
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema hayo jana mjini hapa wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mradi kujenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo mkubwa wa kilovoti 400 ujulikanao kama “Backbone Transmission Investment Project” ambao unajengwa kutoka Iringa mpaka Shinyanga kupitia Dodoma na Singida.
Alisema mahitaji ya umeme katika mkoa wa Dodoma ni megawati 25.2 na sasa wanajipanga kuhakikisha makao makuu hayo ya nchi yanakuwa na uhakika wa umeme siku zijazo.
Alisema umeme wa megawati 60 utatosha Dodoma.
“Kesho (Leo) kutakuwa na kikao kati ya Wizara ya Nishati, Mamlaka ya Ustawishaji makao makuu (CDA) na Shirika la Umeme (Tanesco) kuona namna ambayo kwa miaka ijayo umeme unakuwa wa kutosha.
Alisema kukamilika kwa miradi ya backbone kutasaidia nchi kuwa na umeme wa uhakika na hata ziada kuuzwa nje ya nchi.
“Tunataka kuingia kwenye power trade (biashara ya umeme) nchi nyingine kama Ujerumani wanauzia umeme Ufaransa kwa nini sisi tusiweze,” alisema Profesa Muhongo.
Alisema Tanzania itakuwa miongoni mwa nchi chache Afrika zenye umeme wa msongo mkubwa kama huo.
Alisema Septemba mwaka huu, Rais John Magufuli atazindua mradi wa ujenzi wa njia ya umeme kutoka Iringa hadi Dodoma ambao umekamilika kwa asilimia 100.
Alisema miradi ya umeme ya kutoka Dodoma hadi Singida na Singida hadi Shinyanga itakamilika Oktoba mwaka huu.
Kwa upande wake, Msimamizi wa Mradi huo, James Khalid alisema mradi huo umegawanywa katika makundi matatu ambapo nguzo kubwa zenye kubeba nyaya za kupitisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 imejengwa kutokea Iringa hadi Dodoma kwa gharama ya dola za Marekani milioni 150, fedha kutoka benki ya dunia na mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.
Sehemu ya pili ni Dodoma hadi Singida inajengwa kwa gharama ya dola za Marekani milioni 169.
Alisema fedha ni kutoka Japan na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na sehemu ya tatu ni Singida hadi Shinyanga ambayo inajengwa kwa gharama ya dola za kimarekani milioni 134.7 kutoka European Investment Bank ambapo miradi hiyo miwili itakamilika Oktoba mwaka huu na kukabidhiwa kwa serikali.
Pia serikali ya Tanzania ilitoa fedha za kulipa fidia Sh bilioni 23. Mradi huo unafadhiliwa kwa pamoja kati ya serikali ya Tanzania, Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Benki ya Exim ya Korea na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) ambapo wawakilishi wake walikuwa kwenye ziara hiyo ya Waziri.
chanzo;habarileo.

Comments