Imedaiwa kuwa Jordan na Uingerea zinashirikiana kwa siri kuisaidia Kenya kukabiliana na kundi la kigaidi la Al Shabab.
Tovuti ya Middle East Eye ‘imefichua’ habari hiyo na kusema Jordan na Uingerea pia zimetuma vikosi vya kijeshi Libya kukabiliana na magaidi wa kundi la kitakfiri wa Daesh au ISIS.
Tovuti hiyo imemnukulu Mfalme Abdullah II wa Jordan akibainisha hayo wakati alipokutana na wabunge wa Baraza la Kongresi la Marekani mwezi Januari.
Mfalme huyo alidokeza kuwa nchi yake ina “kikosi cha haraka ambacho kitashirikiana na wanajeshi wa Uingereza na Kenya” ambacho kitaingia Somalia na kukabiliana na magaidi wa al Shabab.
Mfalme wa Jordan amenukuliwa akisema kuwa kuna haja ya kukabiliana na magaidi wa al Shabab kwani hivi sasa magaidi wa kundi hilo wanaelekea Libya na kujiunga na kundi la kigaidi la ISIS.
Serikali ya Kenya tayari imeshatuma wanajeshi zaidi ya 3,000 nchini Somalia tokea mwaka 2011 baada ya magaidi wa al-Shabab kutekeleza hujuma kadhaa ndani ya ardhi ya Kenya.
Magaidi wa al Shabab wameendeleza mashambulizi yao Kenya na pia kuwaua wanajeshi wa Kenya nchini Somalia ili kuishinikiza serikali ya Nairobi iondoe askari wake Somalia. Askari wa AMISOM wako nchini Somalia kuangamiza kundi la al Shabab na kuilinda serikali ya Somalia.
Katika wiki za hivi karibuni jeshi la Kenya limetangaza kuwaangamiza makumi ya magaidi wa al Shabab katika mapigano nchini Somalia.
chanzo;kiswahili.irib.ir
Comments